Mkuu wa Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Morogoro, SSP Gabriel Chiguma, amewaonya madereva wa Serikali kuacha tabia ya kuvunja sheria za barabarani kwa kisingizio cha vyeo au kinga ya nafasi zao.
Akizungumza na madereva wa Taasisi ya Kudhibiti Ubora wa Mbegu Tanzania (TOSCI), SSP Chiguma amesisitiza kuwa hakuna mtumishi wa umma aliye juu ya sheria na kuwataka kutii kanuni na taratibu zote ili kuepusha ajali zinazosababisha vifo, majeraha, na uharibifu wa mali za Serikali.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TOSCI, Bw. Nyasebwa Chimagu, amewataka madereva hao kuwa na nidhamu ya hali ya juu katika kulinda rasilimali za umma na maisha ya wananchi wanapokuwa barabarani.
Amesisitiza kuwa uzingatiaji wa sheria ni msingi wa ujenzi wa taifa lenye nguvu kazi na maendeleo endelevu, huku menejimenti ya taasisi hiyo ikihimiza madereva wa kanda zote kuishi kwa mfano bora katika usalama wa barabarani.
Chanzo; Itv