Mohamed Kisingwe ambaye ni mkazi wa Zingibari, Wilaya ya Mkinga pia kazi yake ni dereva bodaboda, anadaiwa kufariki dunia baada ya kuishiwa nguvu alipokuwa akiwakimbia maofisa wa Mamlaka ya Kupambana na Kudhibiti Dawa za Kulevya (DCEA) mkoani Tanga.
Kisingwe alifariki dunia akiwa anapatiwa matibabu katika Hospitali ya Wilaya ya Mkinga baada ya kukamatwa akidaiwa kusafirisha mirungi.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Almanus Mchunguzi, amesema tukio hilo lilitokea Februari 7, 2026 katika eneo la Maandakini, Kata ya Nayomboni, Wilaya ya Mkinga.
Kwa mujibu wa Kamanda Mchunguzi, maofisa wa DCEA walikuwa wakitekeleza operesheni maalumu kufuatia taarifa za kiintelijensia kuhusu watu waliokuwa wakijihusisha na usafirishaji wa mirungi katika eneo hilo.
“Maofisa wa DCEA walimkuta mtu huyo akiendesha pikipiki namba MC 723 EFD akiwa amebeba mirungi. Walipomsimamisha kwa ajili ya ukaguzi, alisimamisha pikipiki na kuanza kukimbia akijaribu kukwepa kukamatwa,” amesema Kamanda Mchunguzi.
Chanzo; Eatv