Shaban Juma (25), mkazi wa Kijiji cha Samamba, Kata ya Puma, Tarafa ya Ihanja, Wilaya ya Ikungi mkoani Singida, amehukumiwa kifungo cha miaka mitatu jela, baada ya kupatikana na dawa za kulevya aina ya bangi misokoto 11 yenye uzito wa gramu 11.
Hukumu hiyo ilitolewa na Mahakama ya Mkoa wa Singida mbele ya Hakimu Alocy Masua, kufuatia ushahidi uliowasilishwa Mahakamani kuthibitisha kosa hilo.
Kwa mujibu wa upande wa mashtaka, mshtakiwa alikamatwa Januari 16, 2026 katika Kijiji cha Samamba na askari wa Jeshi la Polisi wakiwa katika operesheni ya kudhibiti Dawa za Kulevya.
Akisoma hukumu, Hakimu Masua amesema adhabu hiyo inalenga kutoa funzo kwa mshtakiwa na jamii kwa ujumla, huku akisisitiza kuwa Mahakama haitavumilia vitendo vya matumizi na usambazaji wa dawa za kulevya vinavyoathiri ustawi wa jamii.
Chanzo; Itv