Mwanafunzi wa kidato cha nne katika Shule ya Sekondari Chief Mang'enya iliyopo wilayani Muheza mkoani Tanga, Abdallah Msenga amefariki dunia baada ya kugongana kichwa na mchezaji wa timu pinzani wakati wakigombea mpira golini.
Tukio hilo limetokea wakati wa mechi ya ligi ya ndani ya shule hiyo iliyokuwa ikizikutanisha timu za wanafunzi wa kidato cha nne mkondo wa AB na CB.
Akidhibitisha kutoka kwa tukio hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa Tanga Almanus Muchunguzi, amesema tukio hilo limetokea Februari 22, mwaka huu wakiwa uwanjani ndani ya shule hiyo.
Kamanda Muchunguzi amesema mwanafunzi huyo alikuwa akigombea mpira na mchezaji mwenzake wa timu pinzani, Abdallah Bakari, ndipo walipogongana vichwa na kusababisha marehemu kuanguka chini.
“Waligongana na marehemu aligonjwa sehemu ya kushoto, na kukimbizwa katika hospitali teule ya Wilaya ya Muheza ingawa alipoteza maisha wakati akipatiwa matibabu,” amesema.
Chanzo; Nipashe