Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Geita imefyeka ekari tatu za bangi zilizokuwa zimepandwa kwa siri ndani ya Hifadhi ya Msitu wa Geita-Lwamgasa.
Watu wasiofahamika walivamia hifadhi hiyo na kuendesha kilimo hicho haramu kwa kuchanganya na zao la mahindi ili kukwepa kubainika, hali iliyomlazimu Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Geita, Bi. Lucy Beda, kutoa onyo kali kwa wananchi wanaovamia hifadhi za misitu kufanya shughuli za kijinai.
Mhifadhi Mkuu wa shamba hilo la miti, Aloyce Paschal, amethibitisha kuwa tayari wanamshikilia mtu mmoja anayedhaniwa kuwa kinara wa kilimo hicho, huku msako mkali ukiendelea kuwapata wahusika wengine.
Viongozi wa vijiji vinavyozunguka hifadhi hiyo wameeleza kuwa wavamizi hao wamekuwa wakifanya shughuli hizo usiku wa manane ili kukwepa mkono wa sheria, jambo linaloashiria hitaji la kuimarisha ulinzi na ushirikiano kati ya walinzi wa misitu na jamii inayozunguka hifadhi.
Chanzo; Itv