Mbunge wa Kinondoni, Abbas Tarimba, amehoji bungeni serikali haioni haja ya kuweka sharti la kisheria la watoto wakubwa kutunza wazazi wao wasiojiweza.
Ambapo akijibu swali hilo kwenye kipindi cha maswali na majibu bungeni leo Januari 28, 2026, Naibu Waziri Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Makundi Maalumu, Mhandisi MaryPrisca Mahundi, amesema serikali inatambua umuhimu wa familia na jamii kuchukua jukumu la kulea wazee, na huu ndio msingi wa mila na desturi zetu Watanzania.
“Katika kuimarisha huduma na matunzo kwa wazee, serikali imefanya mapitio na kutunga Sera ya Taifa ya Wazee ya mwaka 2003, Toleo la Mwaka 2024.
“Sera hiyo inatoa wajibu kwa familia na jamii kusimamia matunzo ya wazazi. Sera hii imeweka msisitizo wa kuimarisha mfumo wa kisheria utakaolinda na kuendeleza wazee ambao pamoja na mambo mengine utawezesha uwajibikaji wa jamii na Watoto kuwatunza wazee wao.
“Napenda kutoa wito kwa wazazi kuwekeza kwenye malezi ya watoto na siyo matunzo peke yake kwani inaendeleza ukaribu na muunganiko imara kati ya wazazi na watoto.
“ Mzazi anapobeba jukumu la malezi na matunzo ya watoto wake kikamilifu hujenga msingi imara kwa mtoto kumhudumia mzazi wake anapozeeka,” amesema Naibu Waziri.
Chanzo; Eatv