Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ameunda Tume Huru ya Uchunguzi kwa ajili ya kuchunguza matukio yaliyotokea Nchini kabla na baada ya Uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba 29, 2025.
Tume hiyo imeundwa hii leo ikiongozwa na Jaji Mkuu Mstaafu wa Mahakama ya Tanzania, Mohamed Chande Othman ambaye atakuwa Mwenyekiti akiwaongoza Wajumbe saba akiwemo Profesa Ibrahim Hamis Juma, Jaji Mkuu Mstaafu wa Mahakama ya Tanzania, Balozi Ombeni Yohane Sefue, Mwanadiplomasia na Katibu Mkuu Kiongozi Mstaafu, Balozi Radhia Msuya Mwanadiplomasia na Balozi Mstaafu, Balozi Luteni Jenerali Paul Meela ambaye ni Mwanadiplomasia na Balozi Mstaafu, IGP Mstaafu Said Ally Mwema, Balozi Mstaafu David Kapya pamoja na Dkt. Stergomena Lawrance Tax.
“Rais wa jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mamlaka aliyonayo chini ya kifungu cha tatu cha sheria ya Tume za Uchunguzi, sura ya 32, ameunda Tume ya Huru ya kufanya uchunguzi wa matukio ya uvunjifu wa amani yaliyotokea Nchini wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu uliofanyika oktoba 29, 2025” imeeleza taarifa Iliyotolewa na Katibu Mkuu Kiongozi Dkt. Moses Kusiluka.
Chanzo; Millard Ayo