Katika kipindi cha mwezi mmoja, Jeshi la Polisi Mkoa wa Tanga limefanikiwa kuwakamata jumla ya watu 55 wanaodaiwa kujihusisha na makosa mbalimbali ,yakiwemo makosa yanayohusisha nyara za Serikali.
Mafanikio hayo yametokana na operesheni maalum zilizofanywa na Jeshi la Polisi katika maeneo mbalimbali ya mkoa, kupitia doria za mara kwa mara na misako ya kushtukiza, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha usalama wa raia na mali zao.
Akizungumza na waandishi wa habari kuhusu operesheni hiyo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, ACP Almachius Muchunguzi, amesema mafanikio hayo yametokana na juhudi za makusudi za kuimarisha ulinzi na usalama pamoja na ushirikiano mzuri uliopo kati ya Jeshi la Polisi na wananchi.
Jeshi la Polisi pia limefanikiwa kukamata pikipiki 50 zinazodaiwa kuhusishwa na matukio ya uhalifu, ambapo kati ya hizo, pikipiki 28 hazikuwa na namba halali za usajili.
Jeshi la Polisi limewataka wananchi kuendelea kushirikiana na Jeshi hilo kwa kutoa taarifa za uhalifu na wahalifu likisisitiza ushirikiano huo ni msingi muhimu katika kudumisha amani na usalama katika Mkoa wa Tanga.
Chanzo; Clouds Media