Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amesema Mashujaa wa Vita ya Majimaji wanapaswa kuenziwa kwa kuimarisha nidhamu ya utendaji kazi, kupinga masuala ya ukabila na kutambua wajibu wa pekee wa kulitetea na kulipigania Taifa.
Makamu wa Rais amesema hayo, wakati wa kilele cha Tamasha la 17 la Kumbukizi ya Miaka 120 ya Mashujaa wa Vita ya Majimaji, lililofanyika katika Viwanja vya Makumbusho ya Vita ya Majimaji, Songea mkoani Ruvuma.
Amesema ni muhimu kuwaenzi mashujaa hao kwa kuendelea kusimamia umoja ili kuhakikisha makabila yote yanakuwa Taifa moja, kufanya kazi kwa bidii kuijenga Nchi, pamoja na kupinga vitendo vya rushwa na kutenda haki.
Ameongeza kwamba, Mashujaa wa Vita ya Majimaji waliweka pembeni ubinafsi kwa kuunganisha makabila zaidi ya 30 ili kuweza kupambana na wakoloni na hivyo kutengeneza mustkabali mzuri wa maisha ya sasa.
Makamu wa Rais, amesema kumbukizi ya Mashujaa wa Vita vya Majimaji ni muhimu katika kuwezesha kizazi cha sasa na kijacho, kuona na kujifunza jinsi ambavyo mashujaa hao walivyojitolea maisha yao katika kulinda heshima, utu na rasilimali za Taifa.
Awali, Makamu wa Rais alishiriki tukio la uwekaji wa silaha za jadi katika mnara wa kumbukumbu ya Mashujaa wa Vita ya Majimaji pamoja na kuweka shada la maua katika makaburi waliozikwa mashujaa hao.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Makambusho ya Taifa Dkt. Noel Lwoga, amesema pamoja na kufanya kumbukizi ya kuwaenzi Mashujaa wa Vita ya Majimaji, lakini pia malengo mengine ni kurithisha urithi wa historia , mila na desturi kwa kizazi cha sasa na baadaye, kuibua na kuendeleza fursa za utalii na uchumi zinazotokana na historia na utamaduni pamoja na kuelimisha umma wa Watanzania umuhimu wa kutunza na kuhifadhi urithi wa Taifa.
Chanzo; Itv