Kufuatia malalamiko ya wateja wa umeme wa Luku kuisha haraka katika matumizi, Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) limefanya ukaguzi wa kitaalamu na kubaini, tatizo hilo linasababishwa na mifumo mibovu ya umeme.
Baada ya kupokea malalamiko hayo, Tanesco, iliwalazimu kufanya ukaguzi wa kitaalamu katika baadhi ya nyumba ili kubaini chanzo cha tatizo hilo.
Matokeo ya awali yanaonesha kuwa, katika matukio mengi, tatizo siyo mita za umeme, bali ni mifumo mibovu ya umeme (wiring) majumbani.
Pia, kukosekana kwa elimu sahihi ya matumizi ya umeme na uharibifu wa mifumo ya umeme katika nyumba nyingi, kumetajwa kuwa chanzo cha ongezeko la matumizi ya umeme, ajali za moto na upotevu wa mali na maisha.
Akizungumza leo Januari 27, 2026 baada ya kufanya uchunguzi katika nyumba zilizowasilisha malalamiko, mhandisi wa Tanesco, Ally Mbonde amesema wamefanya uchunguzi katika baadhi ya nyumba na kubaini kuwa, mita nyingi ziko salama na zinapima kwa usahihi.
Chanzo; Mwananchi