Mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la Bw. Matondo Kilugala Malanda ambaye ni mmiliki wa kampuni ya Matondo Breweries Investment Limited iliyopo wilaya ya Bukombe mkoani Geita, amefikishwa katika Mahakama Kuu ya mkoa huo kwa tuhuma mbalimbali za kikodi na kusomewa mashtaka nane yanayomkabili.
Bw. Matondo amesomewa mashitaka yake mbele Hakimu Mkazi wa Mahakama Kuu Geita Mhe. Cleofas Waane Februari 10, 2026 ambapo shauri lake limeanza kusikilizwa rasmi.
Akizungumza kuhusu shauri hilo, Wakili wa Serikali Bw. Emmanuel Cheneko amesema mtuhumiwa huyo anakabiliwa na tuhuma nane za kikodi, ikiwemo kuanza uzalishaji bila kuwa na leseni halali na matumizi ya stempu bandia.
Tuhuma nyingine ni kukutwa na bidhaa zinazopaswa kulipiwa ushuru wa bidhaa bila kulipiwa ushuru huo, pamoja na kushindwa kuandaa na kuwasilisha ritani za ushuru wa bidhaa kama inavyotakiwa kisheria.
Aidha, Meneja wa Idara ya Upelelezi wa Kodi Kanda ya Ziwa, Bw. Joel Mbilinyi, amewakumbusha wazalishaji wa vinywaji changamshi kuwa pamoja na kupata usajili kutoka BRELA, wanapaswa pia kupata leseni ya uzalishaji kutoka TRA kwa mujibu wa sheria, ili kuepuka kuchukuliwa hatua za kisheria.
Ametoa rai kwa wasambazaji na walaji kuomba risiti za EFD wanaponunua bidhaa na kuhakiki stamp kwa kutumia programu ya hakiki stamp hali itakayosaidia kutokupotea kwa mapato, kulinda afya za walaji na kuleta usawa katika ushindani sokoni.
Chanzo; Clouds Media