Search

Saved articles

You have not yet added any article to your bookmarks!

Browse articles

GDPR Compliance

We use cookies to ensure you get the best experience on our website. By continuing to use our site, you accept our use of cookies, Privacy Policy, and Terms of Service.

Pingamizi la Lissu Lakubaliwa Mahakamani

Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Dar es Salaam imekubaliana na pingamizi la Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Tundu Lissu, kwamba kizimba maalum kilichotengenezwa kwa ajili ya shahidi wa siri kifanyiwe marekebisho ili majaji waweze kumuona na kutathmini ipasavyo ushahidi wake.

Uamuzi huo umetolewa na jopo la majaji watatu wakiongozwa na Jaji Dunstan Ndunguru, akisaidiana na Jaji James Karayemaha na Jaji Ferdinand Kiwonde, baada ya kusikiliza hoja za pande zote. Upande wa Jamhuri ulidai kuwa kizimba hicho kilichotengenezwa kwa mbao (kiboksi) kiliruhusu majaji kumuona shahidi bila tatizo.

Akisoma uamuzi huo, Jaji Ndunguru amesema kizimba hicho hakikidhi matakwa ya Kanuni ya 3 ya Ulinzi wa Mashahidi, kwani kimejengwa kwa namna inayowazuia majaji kumuona shahidi moja kwa moja.

“Namna kilivyojengewa ni kweli hakikidhi Kanuni ya 3 ya Ulinzi wa Mashahidi na kinafanya majaji washindwe kutathmini ushahidi wake kwa sababu haimuoni. Tunakubaliana na hoja ya mshtakiwa,” amesema Jaji Ndunguru.

Amefafanua kuwa kwa mujibu wa kanuni hiyo, kizimba maalum kinapaswa kuwa sehemu iliyoandaliwa mahususi kumuwezesha shahidi anayeitoa ushahidi kuonekana na jaji au hakimu anayesikiliza shauri.

Hata hivyo, mahakama imekubaliana na pingamizi hilo moja tu kuhusu kizimba, na kuyatupilia mbali pingamizi manne yaliyowasilishwa na Lissu, likiwemo la kupinga matumizi ya Kanuni za Kuficha Mashahidi kwa madai kuwa hazikuchapishwa kwenye Gazeti la Serikali.

“Upande wa Jamhuri uliwasilisha nakala ya Gazeti la Serikali lililochapisha kanuni hizo. Mahakama imeona pingamizi la kwanza tu ndilo lenye mashiko; manne yamekataliwa,” amesema Jaji Ndunguru.

 

 

Chanzo; Nipashe

Kuhusiana na mada hii: