Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar imesema imepokea malalamiko mazito kuhusu tuhuma za adhabu iliyopitiliza kwa mwanafunzi wa kidato cha nne katika Shule ya Sekondari ya Indian Ocean iliyopo visiwani humo.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Wizara hiyo leo, haikubaliani na tukio hilo iwapo limetokea, likielezwa kuwa ni ukiukwaji wa sheria na kanuni za utoaji wa adhabu kwa wanafunzi shuleni.
Wizara imeeleza kuwa walimu pamoja na uongozi wa shule wana wajibu wa kufuata miongozo na taratibu zilizowekwa kuhusu namna ya kutoa adhabu, na kwamba haitavumilia vitendo vinavyokiuka misingi ya haki na ustawi wa wanafunzi.
“Wizara imeanza kulifuatilia tukio hilo kwa ukaribu na hatua stahiki kwa mujibu wa sheria zitajukuliwa endapo itabainika kuwa kulikuwa na ukiukwaji wa taratibu,” imesema sehemu ya taarifa hiyo.
Chanzo; Nipashe