Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imejibu ripoti iliyotolewa na Shirika la Kutetea Haki za Binadamu la Human Rights Watch (HRW), iliyodai kuwa ukandamizaji wa kisiasa umeongezeka wakati taifa hilo linapoelekea kwenye Uchaguzi Mkuu uliopangwa kufanyika Oktoba 29, 2025.
Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa amesema, taarifa iliyotolewa na HRW Septemba 29, 2025, kuwa sio sahihi na ni za kupotosha huku ikikanusha pia taarifa za kutekwa kwa raia nchini humo.
“ Madai kuwa kuna kupungua kwa uhuru wa kisiasa kuelekea uchaguzi mkuu wa 2025 si ya kweli,” Taarifa hiyo imesema.
“Katiba ya nchi inatoa haki ya kuishi, usalama na uhuru kwa kila Mtanzania,” Taarifa hiyo imeongeza.
Ikijibu taarifa ya HRW, Tanzania imesema ipo tayari wakati wote kushirikiana na taasisi yoyote inayotafuta taarifa sahihi.
Taarifa ya HRW ilisema kuwa mamlaka nchini Tanzania zimekandamiza upinzani na wakosoaji wa chama tawala, zinanyamazisha vyombo vya habari, na zimeshindwa kuhakikisha uhuru wa tume ya uchaguzi.
“Mamlaka ya Tanzania inapaswa kuchukua hatua za haraka kulinda uadilifu wa uchaguzi wa Oktoba, ambao kwa sasa uko katika hatari kubwa,” alisema Nomathamsanqa Masiko-Mpaka, mtafiti wa Afrika katika Human Rights Watch.
“Mamlaka inahitajika kujizuia kukandamiza upinzani na vyombo vya habari, na badala yake hushiriki katika mageuzi yenye maana ili kuhakikisha uchaguzi huru, wa haki na wa kuaminika,” Taarifa ya HRW ilisema.
Tanzania imelaumu shirika hilo kwa kutoa taarifa za aina hiyo bila kuipatia fursa ya kujibu kabla ya kuchapishwa.
Tanzania imesema kuwa imejipanga kuhakikisha haki za binadamu, demokrasia, utawala bora na sheria vinaheshimiwa kabla, wakati na baada ya uchaguzi mkuu wa 2025.
Chanzo: Bongo 5