Spika wa Bunge la Tanzania Mussa Zungu ametoa ufafanuzi kuhusu taarifa zilizosambaa kwenye baadhi ya vyombo vya habari zikidai kuwa wabunge wawili wa CCM Ahmed Shabiby (Gairo) na Kangi Lugola (Mwibara) kuitwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kufuatia michango yao waliyotoa Bungeni.
Akitoa ufafanuzi huo Zungu amesema kuwa Ofisi ya Spika haijapokea wito wowote wa kumtaka mbunge aende TAKUKURU wala Spika hajatoa kibali kwa mbunge yeyote kuomba au kuitwa kuhojiwa na TAKUKURU kwa sababu ya michango ya Bungeni.
“Kanuni za kudumu za Bunge zimeweka wazi masuala yasiyoruhusiwa kujadiliwa bungeni na endapo ukitokea ukiukwaji kiti kinaweza kuelekeza kufutwa kwa mchango usioruhusiwa au kumtaka mbunge kufuta mchango wake iwapo mbunge atakaidi maelekezo ya kiti anaweza kupelekwa kwenye kamati ya Bunge kwa ajili ya uchunguzi.” Mussa Zungu - Spika wa Bunge la Tanzania
Spika Zungu amesisitiza kuwa masuala yote yanayohusu mienendo ya wabunge ndani ya Bunge yanapaswa kushughulikiwa kwa kuzingatia Kanuni za Kudumu za Bunge bila kuingiliwa na taasisi nyingine pasipo utaratibu rasmi wa kibunge.
Chanzo; Millard Ayo