Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) limesema limeguswa na kuumizwa sana na matukio ya vurugu zilizosababisha vifo na majeruhi na kupotea kwa mali October 29,2025 na kusema linakemea matukio hayo yanayomchukiza Mungu.Taarifa iliyotolewa
na Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Askofu Dkt. Alex Gehaz Malasusa imesema Kanisa hilo linatoa pole kwa Jamii na Familia zilizopoteza Wapendwa wake kwa kuuawa au bado hawajapatikana bila maelezo ya kuridhisha na limetoa pole kwa uharibifu wa mali za umma na za binafsi uliofanyika.
“Kanisa linawaombea Wafiwa wote, Majeruhi, Watu ambao bado hawajapatikana na wanaoshikiliwa bila hatia na linaomba toba na rehema kwa Mungu ili Nchi yetu iliyoshuhudia umwagaji wa damu za Watu ipate kuokolewa dhidi ya ghadhabu ya Mungu juu ya chukizo hili na ipate neema ya kurejea katika amani”
Kufuatia mauaji hayo Kanisa hilo limetoa wito kwa Serikali kusikiliza na kushughulikia malalamiko ya Wananchi kwa namna ya kujenga umoja wa kitaifa na utengamano wa kijamii, Serikali kuwatendea haki Raia wote waliopoteza maisha au walioathiriwa “Kanisa linakumbusha kuwa matumizi ya nguvu ya kupita kiasi kwa yeyote hayawezi kuleta baraka na la Mungu linaonya kuwa ‘hasira ya Mwanadamu haiitendi haki ya Mungu’ (Yakobo 1:20)“.
Chanzo; Millard Ayo