Jeshi la Polisi Mkoani Kigoma linatarajia kuanza msako mkali dhidi ya watu wanaochochea vurugu kupitia migogoro ya wakulima na wafugaji kufuatia mauaji ya mkazi mmoja wa Kitongoji cha Ilunde, Wilayani Uvinza.
Marehemu huyo, ambaye utambulisho wake haujafahamika mara moja, alifariki dunia baada ya kupigwa na jembe kichwani huku wengine wawili wakijeruhiwa vibaya na kukimbizwa hospitali katika shambulio lililohusisha silaha za jadi.
Tukio hilo linahusishwa na migogoro ya ardhi kati ya wawekezaji na wananchi wa eneo hilo ambao wamekuwa wakilalamikia ukosefu wa mpango bora wa matumizi ya ardhi.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kigoma, SACP Filemon Makungu, pamoja na Mkuu wa Mkoa, Balozi Simon Sirro, wameingilia kati suala hilo huku wananchi wakisisitiza kuwa kutopangwa vizuri kwa maeneo ya kilimo na ufugaji ndiko kunakochochea mapigano hayo ya mara kwa mara.
Chanzo; Itv