Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Musoma, imempa muda wa siku 30, aliyekuwa mwalimu, Kasoga Mangire, kufungua shauri la maombi ya mapitio kupinga uamuzi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuridhia kufukuzwa kwake kazi.
Uamuzi huo umetolewa Januari 30, 2026 na Jaji Marlin Komba baada ya kukubaliana na maombi ya Kasoga kuongezewa muda wa kufungua shauri hilo na nakala yake kuwekwa kwenye mtandao wa Mahakama.
Katika maombi hayo, wajibu maombi ni Katibu Mkuu wa Tume ya Utumishi wa Walimu Tanzania (TSC), Rais pamoja na Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Mahakama imesema kuwa mwombaji ameibua hoja nzito za kisheria zinazostahili kusikilizwa katika shauri la mapitio ya Mahakama ambapo mwombaji huyo anaiomba Mahakama ibatilishe uamuzi wa kumfukuza kazini na kuamuru mamlaka husika kutekeleza wajibu wao kwa mujibu wa sheria.
Jaji Komba amesema Mahakama imejiridhisha kuwa madai ya mwombaji, hususan kuhusu kunyimwa haki ya kusikilizwa, yana msingi wa kisheria unaohitaji uchunguzi wa kina, hivyo kuruhusu maombi hayo ya mapitio yafunguliwe tangu tarehe ya hukumu.
Chanzo; Mwananchi