Mahakama Kuu ya Zanzibar haijatoa zuio lolote kwa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) kutekeleza zoezi la kuteketeza nyaraka zilizotumika katika Uchaguzi Mkuu, kinyume na taarifa zinazosambazwa na chama cha ACT Wazalendo.
Akizungumza na Nipashe, mmoja wa watendaji wa Mahakama Kuu ambaye hakutaka kutajwa jina lake, amesema taarifa hizo hazina ukweli wowote na kwamba mahakama bado haijatoa uamuzi wowote kuhusu suala hilo.
Amesema Mahakama Kuu inatarajiwa kutoa uamuzi wake rasmi Februari 10 mwaka huu, hivyo ni mapema kwa upande wowote kudai kuwepo kwa katazo la mahakama.
“Taarifa zinazosambazwa kuwa mahakama imetoa zuio kwa ZEC kuteketeza nyaraka za uchaguzi si za kweli. Mpaka sasa hakuna uamuzi wowote uliotolewa,” amesema Mtendaji huyo.
Mkurugenzi wa Uchaguzi wa ZEC, Thabit Idarous Faina, amesema tume hiyo haijapokea taarifa yoyote rasmi kutoka Mahakama Kuu inayozuia utekelezaji wa zoezi la kuangamiza nyaraka za uchaguzi.
Chanzo; Nipashe