Alphonce Kaishozi, dereva wa daladala anayetuhumiwa kumgonga askari wa usalama barabarani, Tumsifu Kileo amekamatwa baada ya kukimbia na kujificha mkoani Kagera.
Dereva huyo alikamatwa Februari 14, 2026 katika kijiji cha Rubare, Wilaya ya Bukoba Vijijini mkoani Kagera alikokuwa amekimbilia baada ya tukio hilo.
Kwa mujibu wa taarifa ya Jeshi la Polisi mkoani Mwanza iliyotolewa jioni ya Februari 16, 2026, jitihada za kumtafuta dereva huyo zilianza baada ya ajali iliyotokea Februari 10, 2026 saa 2:00 asubuhi katika mzunguko wa Mwanza Hoteli katikati ya Jiji la Mwanza.
“Na sasa hivi tunapoongea ameishaletwa katika Mkoa wa Mwanza anahojiwa na amekiri kuhusika na ile ajali kwa hiyo taratibu kwa mujibu wa sheria za kumfikisha mahakamani zinaendelea kufanyika… atafikishwa mahakamani mara moja tutakapokuwa tumekamilisha uchunguzi wetu na taratibu zetu kwa mujibu wa sheria,”ameeleza Mutafungwa.
Kuhusu mmiliki wa daladala hiyo, Jeshi la Polisi limesema anaendelea kushikiliwa katika Kituo cha Polisi Nyamagana kwa mahojiano, kwa madai ya kumkabidhi gari dereva ambaye hakuwa ametunza kumbukumbu zake kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu za usalama barabarani.
Chanzo; Mwananchi