Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani Wilaya ya Momba, Mrakibu Msaidizi wa Polisi (ASP) Fidelia Kasongwa, amelikamata gari aina ya Toyota Hiace lenye namba za usajili T 577 BNN, linalomilikiwa na Shule ya Msingi HQ iliyopo Tunduma, kwa kosa la kuwabeba wanafunzi 40 badala ya 15 kwa msongamano mkubwa, kinyume na sheria na taratibu za usalama barabarani.
Tukio hilo limetokea Januari 03, 2026 katika eneo la Kilimanjaro, Mji wa Tunduma, Wilaya ya Momba, Mkoa wa Songwe, ambapo gari hilo dogo lilikutwa likisafirisha wanafunzi wengi kupita kiasi, hali iliyohatarisha usalama wa maisha yao.
Kutokana na kosa hilo, gari hilo lilipigwa faini kwa mujibu wa sheria na kutolewa maelekezo ya kutoruhusiwa kuendelea na safari na lisitowe huduma yoyote hadi pale litakapofanyiwa matengenezo stahiki na kukaguliwa na Mkaguzi wa Magari wa Jeshi la Polisi, ili kuthibitisha kuwa lipo katika hali salama na linakidhi vigezo vya usalama barabarani.
Jeshi la Polisi kupitia Kikosi cha Usalama Barabarani linaendelea kusisitiza utii wa sheria za usalama barabarani, hususan kwa vyombo vinavyosafirisha wanafunzi, kwa lengo la kulinda maisha ya watoto na kuzuia ajali zinazoweza kuepukika.
Chanzo; Bongo 5