Jeshi la Polisi Mkoa wa Njombe limesema kuwa, kwa kushirikiana na raia wema limefanikiwa kumkamata mama aliyetelekeza mtoto mdogo ndani ya ofisi ya Basi la Superfeo.
Mtuhumiwa ambaye amefahamika kwa jina la Zainabu Mshamu Abdallah (20), mkazi wa mtaa wa Mji Mwema katika mahojiano amesema, alitenda kosa hilo baada ya kufukuzwa kwenye nyumba aliyokuwa amepanga na kushindwa kujikimu yeye na mtoto wake.
Taarifa ya Jeshi la Polisi iliyosainiwa na Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Njombe, imewataka wananchi kuacha tabia ya kuwatelekeza watoto, kwani kufanya hivyo ni kosa kisheria na kinyume cha maadili ya Watanzania.
Chanzo; Mwananchi