Kiongozi wa Kanisa Katoliki Duniani, Papa Leo XIV, ametuma salamu za rambirambi kutokana na kifo cha Madhama Kardinali Polycarp Pengo, akimtaja kama mchungaji mwaminifu aliyejitoa kwa dhati kulitumikia Kanisa na Taifa.
Salamu hizo zimewasilishwa kwa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Yuda Thaddeus Ruwa’ichi, akionesha masikitiko yake Baba Mtakatifu na mshikamano wake na waumini wa Tanzania katika kipindi hiki cha majonzi.
Katika ujumbe wake, Papa Leo XIV amesema Kanisa limepoteza kiongozi mwenye busara, aliyesimama imara katika kulinda na kufundisha imani, huku akionesha unyenyekevu na moyo wa huduma kwa watu wa rika zote. “Tunamshukuru Mungu kwa zawadi ya maisha na utumishi wa Kardinali Pengo, aliyetoa mchango mkubwa katika ujenzi wa Kanisa na malezi ya watumishi wake,” sehemu ya ujumbe huo imenukuliwa.
Huduma ya Kiaskofu na malezi ya makleri
Baba Mtakatifu amekumbusha kwa namna ya pekee mchango wa Kardinali Pengo katika malezi akieleza kuwa juhudi zake zimeacha alama isiyofutika katika historia ya Jimbo Kuu la Dar es Salaam na majimbo mengine aliyoyahudumia nchini.
Kwa zaidi ya miongo kadhaa ya utumishi wa Kiaskofu, Kardinali Pengo alihudumu katika majimbo mbalimbali ya Tanzania, akijipambanua kwa msimamo thabiti wa mafundisho ya Kanisa na juhudi za kuimarisha taasisi za kichungaji, elimu na huduma za kijamii.
Chanzo; Mwananchi