Siku tisa zikiwa zimepita tangu Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kutawatangazia wafanyabiashara wanaofanya shughuli zao maeneo yasiyo rasmi kuondoka, baadhi ya maeneo yameonekana kuanza kupitika kwa sasa tofauti na ilivyokuwa siku za nyuma.
Baadhi ya barabara ambazo zimeanza kupitika ni pamoja na ya Mtaa wa Tandamti, Mkunguni na Nyamwezi yote ikiwa ya kuelekea Soko Kuu la Kariakoo ambapo wananchi wanaopita maeneo hayo wameonekana kufurahishwa na hali ilivyo.
Sambamba na hilo, kumekuwa na urahisi wa vyombo vya moto yakiwemo magari, bajaji kuingia na kutoka bila sokoni humo bila bughdha.
Februari 8, 2026, katika hafla ya ufunguzi wa Soko Kuu la Kariakoo, iliyofanywa na Rais Samia Suluhu Hassan, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila alisema kuanza huduma katika Soko Kuu la Kariakoo kutaambatana na kufunguliwa na barabara zote zinazoingia na kutoka sokoni humo.
Hatua hiyo kwa mujibu wa Chalamila, inalenga kuongeza usalama wa soko hilo, urahisi wa huduma na kurahisisha uokozi inapotokea changamoto.
Alisema tayari ameshazungumza na wafanyabiashara wote kuanzia sasa barabara zote ndani ya soko hilo zitafunguliwa, ingawa anafahamu maelekezo hayo yanaweza kuwa machungu kwa baadhi ya watu.
Chanzo; Mwananchi