Serikali imetangaza hatua mbalimbali za kuboresha usafiri wa wanafunzi katika maeneo ya mijini, huku ikitoa onyo kwa baadhi ya makondakta wa daladala wanaonyanyasa wanafunzi.
Akizungumza na vyombo vya habari jijini Dodoma Februari 4, 2026 Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa amesema Serikali imechukua hatua baada ya kusikiliza kilio cha wanafunzi walioeleza changamoto wanazokumbana nazo ikiwemo kugomewa nauli yao ya Sh200.
Profesa Mbarawa amesema Serikali itaendelea kusimamia utekelezaji wa Sh200 kwa wanafunzi, kuanzisha mabasi maalumu ya wanafunzi nyakati za asubuhi na jioni, pamoja na kutenga mabehewa maalumu katika treni za mijini ili kuongeza usalama na upatikanaji wa usafiri kwa wanafunzi.
Waziri Mbarawa ameielekeza Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (Latra), kupitia Mkurugenzi wake, Dk Habibu Suluo kuhakikisha wanaimarisha udhibiti wa madereva na makondakta kuchukua hatua kali.
Wizara imetoa rai kwa wananchi kuendelea kushirikiana na Serikali kwa kutoa taarifa na ushahidi wa vitendo vinavyokiuka sheria za usafiri wa ardhini kupitia namba za bure zilizopo ubavuni mwa kila daladala.
Chanzo; Mwananchi