Umoja wa Ulaya (EU) umeishutumu TikTok kwa kukihujumu sheria za kidijitali kwa kutumia kile kilichoelezwa kama “muundo unaosababisha uraibu” ikiwemo vipengele vya autoplay na endless scrolling katika hatua za awali za mashitaka yanayolenga kiini cha uendeshaji wa jukwaa hilo.
Wasimamizi wa EU wamesema uchunguzi wao umebaini kuwa TikTok haijafanya vya kutosha kutathmini athari za kiafya kimwili na kisaikolojia za vipengele vyake kwa watumiaji, wakiwemo watoto na watu wazima walio katika mazingira hatarishi.
Tume ya Ulaya imeeleza kuwa inaamini TikTok inapaswa kubadilisha “muundo wa msingi” wa huduma yake.
Tume hiyo ndiyo msimamizi wa Sheria ya Huduma za Kidijitali (Digital Services Act), inayozitaka kampuni za mitandao ya kijamii kulinda watumiaji au kukabiliwa na faini kubwa.
Hata hivyo, TikTok imekanusha vikali madai hayo. Katika taarifa yake, kampuni imesema kuwa matokeo ya awali ya Tume ya Ulaya ni “ya uongo kabisa na hayana msingi wowote”, na ikaahidi kupinga hatua hizo kwa njia zote za kisheria.
Kwa sasa, TikTok imepewa fursa ya kujibu rasmi hoja za Tume. Endapo EU itaendelea na uamuzi wa kutokuzingatia sheria, TikTok inaweza kutozwa faini hadi asilimia 6 ya mapato yake ya kila mwaka duniani.
Kwa mujibu wa Tume ya Ulaya, TikTok inahamasisha matumizi ya muda mrefu kupita kiasi kwa kuwazawadia watumiaji maudhui mapya mfululizo, hali inayodaiwa kupunguza uwezo wa kujidhibiti kwa watumiaji.
Chanzo; Bongo 5