Kijana Bellarmine Mugabe, ambaye ni mtoto wa mwisho wa aliyewahi kuwa Rais wa Zimbambwe, hayati Robert Mugabe, amekamatwa nchini Afrika Kusini kwa tuhuma za kutaka kuua akidaiwa kumpiga risasi mtunza bustani wake.
Tukio hilo ambalo limetokea jana Alhamisi Februari 19, 2026 katika eneo la Hyde Park, jijini Johannesburg, polisi walifika baada ya kutolewa taarifa na wananchi kuwepo milio ya ufyatuaji risasi.
Hata hivyo, Polisi baada ya kufika eneo la tukio na walimkuta mwanamume mwenye umri wa miaka 23 akivuja damu kutokana na jeraha la risasi na walimuwahisha hospitalini ambako hali yake inaelezwa kuwa yupo mahututi.
Msemaji wa Polisi wa Gauteng, Dimakatso Nevhuhulwi amesema wamepata ganda la risasi lililotumika na kikosi cha mbwa wa polisi kiliitwa kusaidia kutafuta bunduki iliyotumika katika tukio hilo.
“Mwathirika ni mtunza bustani na inaonekana hakufika kazini kwa muda fulani, na kulikuwa na mabishano kuhusiana na hilo. Mwathirika alipigwa risasi mara moja,” amesema Nevhuhulwi wakati akizungumza na waandishi wa habari katika eneo la tukio.
Polisi imesema kijana huyo wa Mugabe, mwenye umri wa miaka 28, pamoja na mwanamume mwingine wa miaka 33, walikamatwa. Hivyo, wanamshikilia Bellarmine akikabiliwa na shtaka la kujaribu kuua.
Chanzo; Mwananchi