Search

Saved articles

You have not yet added any article to your bookmarks!

Browse articles

GDPR Compliance

We use cookies to ensure you get the best experience on our website. By continuing to use our site, you accept our use of cookies, Privacy Policy, and Terms of Service.

Akiri Kumua Charlie Kirk Sababu ya Kumchukia

Mwanamume mmoja nchini Marekani, Tyler Robinson mwenye umri wa miaka 22, ameshtakiwa kwa mauaji ya mwanaharakati mashuhuri wa mrengo wa kulia, Charlie Kirk. Kwa mujibu wa waendesha mashtaka katika Kaunti ya Utah, Robinson alikiri kumuua Kirk kupitia barua aliyoiacha nyumbani kwa mpenzi wake pamoja na ujumbe wa maandishi uliotumwa kabla ya tukio hilo.

Wakili wa Kaunti ya Utah, Jeffrey Gray, alisema kuwa Robinson aliacha barua chini ya baobonye (keyboard) kwa ajili ya mpenzi wake, akimweleza kile alichokifanya. Katika barua hiyo, Robinson alinukuliwa akisema: “Nilipata fursa ya kumuondoa Charlie Kirk, na nimeitumia.” Aidha, waendesha mashtaka walieleza kuwa walipata pia ujumbe wa maandishi uliotumwa kwa mpenzi huyo, ambapo mshtakiwa alidai wazi kuwa alimpiga risasi Kirk kwa sababu “namchukia sana.”

Kwa sasa, mshtakiwa anazuiliwa bila dhamana katika kitengo maalum cha makazi kwenye jela ya Kaunti ya Utah. Hatua hiyo imechukuliwa kwa kuzingatia uzito wa mashtaka dhidi yake na hatari inayoweza kutokea iwapo ataachiwa huru. Robinson alifikishwa mahakamani kwa mara ya kwanza Jumanne wiki hii, ambapo mashtaka saba yaliwasilishwa rasmi dhidi yake.

Mashtaka hayo ni pamoja na kosa la mauaji ya kuchochewa, kukutwa na silaha isivyo halali, makosa mawili ya kuzuia haki, makosa mawili ya kuharibu ushahidi, pamoja na kufanya uhalifu wa kutumia nguvu wakati watoto walikuwapo. Mashtaka haya yanaonyesha uzito na ukali wa kesi inayomkabili Robinson.

Charlie Kirk alikuwa mwanaharakati maarufu katika siasa za mrengo wa kulia na mwanzilishi wa shirika la vijana la Turning Point USA. Kifo chake kimeshtua watu wengi ndani na nje ya Marekani, na kuzua mjadala mpana kuhusu usalama wa wanasiasa na wanaharakati katika mazingira ya kisiasa yanayozidi kuwa yenye mvutano.

Uchunguzi wa tukio hilo bado unaendelea, huku mamlaka zikiendelea kukusanya ushahidi na kufanya mahojiano zaidi ili kubaini undani wa mauaji hayo. Familia ya Kirk na wafuasi wake wametoa wito wa haki kutendeka haraka, wakieleza masikitiko yao juu ya tukio hilo la kikatili.

 

Chanzo; Global Publishers

Kuhusiana na mada hii: