Baraza la Mawaziri Zimbabwe limeidhinisha rasimu ya sheria ambayo itamruhusu Rais Emmerson Mnangagwa (83), kuongeza muda wake wa kukaa madarakani hadi angalau mwaka 2030.
Waziri wa Sheria Ziyambi Ziyambi amesema mashauriano ya umma yatafanyika kabla ya mswada huo kuelekea bungeni kwa mjadala.
Imeelezwa kuwa changamoto za kisheria zinaweza kujitokeza kwakuwa wataalam wa kikatiba wanahoji kuwa kura ya maoni inahitajika ikiwa ukomo wa muda utabadilishwa na kwamba marekebisho hayo hayawezi kumnufaisha rais aliyepo.
Rais Mnangagwa, ambaye aliingia madarakani kwa mara ya kwanza mwaka 2017 baada ya mapinduzi ya kijeshi yaliyomuondoa madarakani kiongozi wa muda mrefu Robert Mugabe, alishinda uchaguzi wa urais mwaka uliofuata na muhula wa pili 2023 ingawa matokeo yalipingwa.
Chanzo; Nipashe