Mwanamuziki wa Canada Justin Bieber ametangazwa na Chuo cha Recording Academy kutumbuiza katika hafla ya ugawaji wa Tuzo za Grammy itakayofanyika Jumapili, Februari 1,2026.
Mara ya mwisho Bieber kutumbuiza Grammys ilikuwa 2022, alipopanda jukwaani na Daniel Caesar na Giveon wakiimba wimbo wa ‘Peaches’. Tangu kipindi hicho, msanii huyo alikuwa amejiondoa kwenye shughuli kubwa za maonesho ya moja kwa moja baada ya kusitisha ziara zake, hatua iliyowafanya mashabiki wake kusubiri kwa hamu kurejea kwake.
Mbali na kutumbuiza mwaka huu, Bieber anawania tuzo nne Grammy. Ikiwemo tuzo ya Albamu Bora ya Mwaka kupitia albamu Swag, ambayo ni kazi yake ya kwanza tangu alipoachia Justice mwaka 2021. Pia anawania tuzo za Uimbaji Bora wa Pop, Albamu Bora ya Pop na Uimbaji Bora wa R&B, hali inayoonesha kurejea kwake kwa nguvu katika ramani ya muziki duniani.
Katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita Bieber amekuwa akionekana mara chache hadharani kutokana na kupumzika kufanya muziki kwa muda. Mbali na Grammy pia amepangwa kuwa msanii mkuu katika tamasha la Coachella litakalofanyika Aprili mwaka huu, likiwa ni moja ya matamasha makubwa zaidi kuwahi kuandaliwa, huku tiketi zake zikiisha tangu mwishoni mwa 2025.
Hata hivyo, kabla ya Bieber kutangazwa, Recording Academy tayari ilitangaza wasanii wengine wakubwa akiwemo Sabrina Carpenter, Clipse na Pharrell Williams.
Chanzo; Mwananchi Scoop