Wabunifu wa mavazi Kelly Evara na Muonekano wameiomba Serikali kuongeza uwekezaji kwenye sekta ya mitindo ya mavazi ili kuongeza tija na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.
Katika mazungumzo yao, wameeleza kuwa fashion ni nyenzo muhimu ya kuitangaza Tanzania kimataifa, hususan katika sekta ya utalii, kwa kuwa mavazi hubeba utamaduni, sanaa na utambulisho wa taifa. Hata hivyo, wamebainisha kuwa tasnia hiyo bado inakabiliwa na changamoto kubwa ya ukosefu wa teknolojia ya kisasa, ikiwemo mashine za viwandani ambazo zingesaidia uzalishaji wa haraka, wa kiwango bora na unaokidhi ushindani wa soko la kimataifa.
Kutokana na hatua ya Serikali kusaidia makundi mengine ya sanaa, wabunifu hao wamesisitiza umuhimu wa kuwepo kwa mikopo nafuu na ruzuku maalum kwa wabunifu wa mitindo. Wanasema hatua hiyo itasaidia kukuza vipaji vya ndani, kuongeza ajira kwa vijana na kuiwezesha Tanzania kushindana kikamilifu katika soko la kimataifa la mitindo.
Chanzo; Global Publishers