Muigizaji maarufu kutoka Mexico, Gerardo Taracena, amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 55.
Taracena alijipatia umaarufu mkubwa kupitia filamu maarufu za kimataifa zikiwemo Apocalypto, Man on Fire, The Mexican na Sin Nombre, pamoja na kufikia kizazi kipya cha watazamaji kupitia tamthilia maarufu ya Netflix Narcos: Mexico.
Taarifa za kifo chake zimethibitishwa rasmi Januari 31, 2026 na Chama cha Kitaifa cha Waigizaji cha Mexico (Asociación Nacional de Actores – ANDA), ambacho kimetoa tamko rasmi kikieleza masikitiko makubwa kufuatia msiba huo.
Hata hivyo, chama hicho hakikutoa maelezo ya kitabibu wala sababu ya kifo chake.
Gerardo Taracena alitambulika kimataifa kwa uigizaji wake wenye nguvu, umakini mkubwa na uwepo mzito katika filamu, akijenga taaluma iliyovuka mipaka ya sinema ya Mexico, Hollywood pamoja na majukwaa makubwa ya utiririshaji wa filamu duniani.
Chanzo; Global Publishers