Mwanamuziki mkongwe wa Dansi, Zahir Zorro, ametoa ufafanuzi kufuatia ujumbe aliouandika kwenye akaunti yake ya Facebook ulioibua taharuki kwa mashabiki na wadau wa muziki.
Katika ujumbe uliosambaa kwa kasi mitandaoni, Zorro aliandika: "Nahitaji mashine saba za kuzima moto nizikwe nazo kwanini? Nafahamu niendako."
Pia akaandika: "Chilling Kisota. Marafiki wamenitakia Toba leo. Nisiende na mashine 7 za kuzima moto!"
Kauli hizo zimewafanya wengi kudhani huenda msanii huyo anapitia changamoto za kiafya au maisha.
Mwananchi imezungumza na Zahir Zorro ambapo amesema ujumbe kama huo ni sehemu ya ubunifu wake wa maudhui, akisisitiza kuwa mashabiki hawapaswi kuwa na taharuki.
"Ujumbe ninaoposti kwenye akaunti yangu ya Facebook ni vibonzo. Watu waache taharuki, akaunti yangu ni biashara, mimi ni creator (muundaji), vitu vyote ninavyoweka ninavitengeneza nalipwa na Facebook," amesema Zorro.
Chanzo; Mwananchi Scoop