Mwigizaji na mtayarishaji wa filamu nchini, anayefahamika kupitia filamu Going Bongo, Ernest Napoleon amesema sekta ya filamu Bongo inahitaji maboresho makubwa ili kufikia ushindani wa kimataifa.
Ernest ametoa kauli hiyo leo Februari 18, 2026 wakati akitambulisha tamthilia yake mpya, Nipo Bongo, itakayoonyeshwa kupitia jukwaa la Bongolix, akieleza kuwa matumizi ya njia za mkato katika uzalishaji ndiyo yanayodumaza ubora wa kazi za ndani.
“Kuna ‘shortcut’ nyingi kuanzia bajeti, stori hadi uigizaji. Hiyo ndiyo tofauti yetu na wenzetu. Wao wanafanya kazi kwa uwekezaji mkubwa na maandalizi mazuri, ndiyo maana kazi zao zinakuwa bora,” amesema.
Amesema alishuhudia hali hiyo alipohudhuria tuzo za filamu Afrika Mashariki, ambapo washindi wa vipengele vya tamthilia bora walitoka Kenya na Uganda, jambo linaloonyesha pengo la ubora baina ya Tanzania na nchi hizo.
Ernest pia amegusia changamoto ya nidhamu kwa baadhi ya wasanii, “Kwa Tanzania, mara nyingi nikifika seti naanza kuwapigia wasanii simu ndipo waje. Hii ni moja ya tofauti inayodumaza sekta. Tumeishia hata kutafsiri filamu za wenzetu ambao kiuhalisia hawajatuzidi,” amesema
Chanzo; Mwananchi