China sasa inaonekana kuwa miongoni mwa nchi zinazoongoza duniani kwa mabadiliko makubwa ya teknolojia ya Akili Bandia (AI), baada ya kutengeneza roboti mbalimbali zinazotoa huduma katika sekta tofauti.
Miongoni mwa roboti hao ni wahudumu wa hoteli, wasambazaji wa vyakula mitaani, walinzi wanaotumia kamera za barabarani, wauguzi pamoja na wafanyakazi wa viwandani.
Hatua hiyo imeishtua dunia kutokana na kasi ya mafanikio na mageuzi makubwa ya kiteknolojia yanayoendelea nchini humo kupitia AI.
Hata hivyo, kumekuwepo na hofu na mjadala mpana kuhusu mustakabali wa ajira.
Swali linaloibuka ni kwamba, wafanyakazi watakaopunguzwa kutokana na matumizi ya teknolojia wataelekea wapi hasa ikizingatiwa kuwa China imekuwa ikijulikana kwa nguvu kazi kubwa na gharama nafuu (cheap labour) kulinganisha na nchi za Marekani, Ulaya na maeneo mengine duniani.
Kwa sasa, China inashika nafasi ya pili kwa idadi kubwa ya watu duniani, ikiwa na zaidi ya watu bilioni 1.4, nyuma ya India.
Hali hii inazidisha mjadala kuhusu hatma ya ajira kwa mamilioni ya wananchi wake endapo roboti na mifumo ya AI vitaendelea kuchukua nafasi ya binadamu katika uzalishaji na utoaji huduma.
Maswali mengine yanayoibuka ni pamoja na iwapo kutakuwa na ongezeko la raia wa China kuhamia mabara mengine, hususan Afrika ikiwemo Tanzania, au kama ni mkakati wa muda mrefu wa China kuimarisha ushawishi wake kiuchumi duniani kupitia teknolojia.
Mjadala huu unaendelea kujitokeza katika makongamano na vikao mbalimbali, ndani na nje ya China.
Chanzo; Global Publishers