Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga, amewataka wakulima na wafanyabiashara kuwa waaminifu kwa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala ili kuongeza tija katika mnyororo wa thamani.
Akizungumza mkoani Mwanza, Waziri Kapinga amebainisha kuridhishwa na ongezeko la bei ya choroko kutoka Shilingi 1,200 mwaka jana hadi Shilingi 1,600 kwa kilo mwaka huu, hatua inayotekeleza maono ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kumlinda mkulima.
Ili kuleta ufanisi zaidi, Waziri ameelekeza Bodi ya Stakabadhi za Ghala (WRRB) na Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka (COPRA) kuweka mikakati thabiti ya kuwawezesha wakulima kuanzia hatua ya uzalishaji hadi masoko.
Mkurugenzi wa WRRB, Bw. Asangye Bangu, amesisitiza kuwa mfumo huo sasa unawasaidia wakulima wa Kanda ya Ziwa kupata taarifa sahihi za bei na kutoa rai kwa vyama vya ushirika kulipa fedha kwa wakati.
Kwa upande wao, viongozi wa Wilaya ya Kwimba na Wabunge wa majimbo ya Sumve na Kwimba wameushukuru mfumo huo kwa kurahisisha upatikanaji wa takwimu za mazao na masoko ya uhakika.
Hata hivyo, wameiomba Serikali kuangalia uwezekano wa kupunguza tozo zisizo za lazima kwenye zao la choroko ili kuwapa wakulima faida kubwa zaidi, wakizingatia kuwa ni zao mbadala wa pamba katika maeneo hayo.
Chanzo; Itv