Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) mkoani Mara imeteketeza zaidi ya kilo 700 za bidhaa za magendo, zikiwemo sigara, dawa za binadamu, na vipodozi vilivyopigwa marufuku.
Zoezi hilo limeongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Butiama, Bi. Thecla Mkuchika, kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mara, Kanali Evans Mtambi, ambapo imeelezwa kuwa bidhaa hizo zilikamatwa zikiingizwa nchini kinyume cha sheria kupitia mpaka wa Sirari na njia nyingine zisizo rasmi.
Meneja wa TRA mkoani Mara, Bw. Nasorro Ndembo, amebainisha kuwa ukamataji huo ni matokeo ya operesheni kali zinazolenga kulinda mapato ya Serikali na afya za walaji.
Bi. Mkuchika ametoa onyo kali kwa wafanyabiashara wanaojihusisha na biashara za haramu na magendo kuacha mara moja, huku akiwataka wananchi kutoa ushirikiano kwa vyombo vya dola ili kudhibiti mianya ya ukwepaji kodi inayokwamisha maendeleo ya taifa.
Chanzo; Itv