Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imetoa elimu kwa walipakodi Shinyanga juu ya namna bora ya ulipaji kodi kwa kutumia mfumo wa kielektroniki, unaolenga kuboresha utoaji huduma.
Wakati mafunzo hayo yakitolewa leo shinyanga TRA imesema walipakodi watatumia Mfumo Jumuishi wa Usimamizi wa Mapato ya Ndani (IDRAS) ambao umeunganishwa na akili unde, ili kumsaidia mlipa kodi kuuliza maswali na kupata majibu papo hapo, bila kufika TRA.
Meneja wa TRA Mkoa wa Shinyanga Emmanuel Maro, amesema mfumo huo, utasaidia kuboresha utoaji wa huduma, kuongeza uwazi, uelewa, utunzaji kumbukumbu, kuongeza ufanisi na upatikanaji wa huduma kwa saa 24.
Pia utapunguza malalamiko ya mashine ya EFD, na kuchochea ulipaji kodi kwa hiari.
“Mafunzo haya tumeamua kuyatoa mapema kwa walipa kodi wetu hapa Shinyanga, sababu ifikapo Februari 9 mwaka huu, mfumo huu utaanza kutumika rasmi,” amesema Maro.
Mfumo huo unachukua nafasi ya mifumo mbalimbali iliyokuwa ikitumika awali ndani ya TRA, kwa lengo la kupunguza matumizi ya makaratasi na kuhamishia huduma zote za kodi katika mfumo wa kidijitali.
Chanzo; Nipashe